Sunday 15 September 2019

VIPENGELE MUHIMU VYA FASIHI SIMULIZI



(a) Msimuliaji (fanani); huyu ni mtendaji wa tukio la kifasihi mbele ya hadhira. Tukio laweza kuwa kutamba hadithi, kuimba wimbo au kutoa kitendawili au methali. Huyu ni muhusika anayesana kazi ya fasihi.
 
(b) Hadhira; hawa ni walengwa wa kazi ya fasihi ambao husikiliza na kutazama kinachotendwa na fanani. Hadhira hushiriki kwa namna fulani kwenye kile kinachotendwa iwe ni kuitikia wimbo au kupiga makofi, kutingisha kichwa au mwili. Hadhira humsaidia fanani kujitathimini juu ya kile anachokitenda na mbinu ya utendaji anayoitumia.
(c) Mandhari; hapa ni mahali ambapo matukio ya kifasihi yanatendekea. Mandhari huweza kuwa uwanjani, kichakani, chini ya mti mkubwa au mlimani.

(d) Tukio; hili ni tendo au tukio linalotendwa na fanani kifasihi. Tendo hili laweza kuwa usimuliaji hadithi, vitendawili, kuimba au kutoa methali. Kwenye fasihi simulizi kuna falsafa na mantiki ambayo haipaswi kusahauliwa wala kudharauliwa. Sengo na Kiango (1977) wanasema; fasihi huweza kulinganishwa na mwamvuli unavyokinga amali za maisha ya watu.

Saturday 14 September 2019

KUTUMIA MICHEZO YA JADI KATIKA KUJIFUNZA


Swali Lengwa muhimu: Unawezaje kutumia michezo ya jadi ili kusaidia ujifunzaji wa lugha?
Maneno muhimu: kutafakari; utafiti; michezo ya jadi; mapokeo; mashairi; nyimbo; kuchunguza

Matokeo ya ujifunzaji

Mwishoni mwa sehemu hii, utakuwa umeweza:
  • umetumia michezo ya jadi na ya mahali husika katika kusaidia shughuli za ujifunzaji;
  • umewahamasisha wanafunzi na kuongeza ujasiri wao wa kutumia lugha kwa njia ya michezo, nyimbo na mashairi;
  • umepanua stadi zako mwenyewe katika kutafakari wajibu na uwezo wako kwa kuchunguza thamani ya michezo katika ujifunzaji.
Utangulizi
Baadhi ya walimu ambao wamefundisha kwa miaka 20 ni kama tu wanakuwa na uzoevu wa mwaka mmoja tu, ambao unarudiarudia. Hii ni kwa sababu hawajifunzi tena kwa bidii au hawajiendelezi ili waweze kuwa walimu bora zaidi.
Walimu wazuri ni wale ambao wanapanga kile wanachotaka kukifanya, na mara wanapokifanya, wanarekodi kilichotokea, na kujiuliza wenyewe mafanikio ni yapi na ni wapi panahitaji kuboreshwa. Wanatafakari endapo wanafunzi wamejifunza chochote, na kama wamejifunza, wamejifunza nini? Kwa msingi huu wa ‘tafakari’, wanapanga tena kwa ajili ya shughuli inayofuata. Nyenzo rejea 1: duara la tenda-tafakari huonesha mchakato huu katika muundo wa kielelezo.

Somo la 1

Watoto hawajifunzi tu wakiwa darasani, wanajifunza pia wakiwa wanacheza. Wanajifunza kutoka kwa wengine, kwa kuangalia kile wanachokifanya wengine. Hujifunza kwa kuzungumza, kuimba, kwa kukariri na kwa kushirikishana katika mazungumzo. Unaweza kutumia mchezo ili kufanya ujifunzaji katika darasa lako uwe wa mafanikio na kuziba uwazi kati ya kinachotokea darasani na nje ya darasa.
Katika Shughuli 1, wanafunzi wako wanakuwa kama watafiti, na wanakwenda kwenye uwanja wa michezo (au mahali pengine) ili kurekodi kile wanachofikiri kuwa wataweza kujifunza pale. Wanaporudi darasani wanazungumzia kile ambacho wamekigundua: Unaweza kusikiliza mazungumzo yao ili kuona kile ambacho unafikiri wanafunzi wako wamejifunza uwanjani hapo.

Uchunguzi kifani ya 1: Mwanafunzi wa miaka sita ajifunza na kufundishaKiswahili

Maria ambaye ana umri wa miaka sita anasoma katika shule ambayo
Kiswahili ni lugha inayotumika darasani, ingawa si lugha yake ya kuzaliwa.
Kila siku kwa muda wa wiki nzima, Maria aliweza kuonekana wakati wa mapumziko akiwaangalia watoto wengine wakiruka kamba. Hakujiunga, lakini alisimama karibu ili kuweza kuona na ‘kusikiliza’ wimbo ambao wanafunzi walikuwa wakiuimba. Siku ya kwanza ya wiki ya pili, Maria alikuwa kwenye ile sehemu yake ya kawaida hatua chache kutoka eneo la kuchezea, lakini sasa aliweza kusikika ‘akitoa sauti’ za maneno ya kwenye wimbo.
‘Ruu-ka, ruuu-kia ndani na seeema
Moja-aa mbili-iii, tatuuu,
Ruuu-kia na-a mimi.’
Alirudia maneno haya tena na tena, akijitahidi kuyasema kwa sauti kubwa, kwa wororo na kwa kutumia mkazo tofauti tofauti kwenye sehemu za neno. Alirudia wimbo huu mara kadhaa na kisha kuwasikiliza tena wanafunzi wengine. Alitabasamu, na kuimba tena ule wimbo.Mwishoni alitafuta kamba na kwenda kwa rafiki yake, Migueli. Aliimba ule wimbo, mstari kwa mstari, akimfundisha rafikiye huu wimbo. Alitafsiri yale maneno ya Kiswahili ili rafiki yake aweze kuelewa alichokuwa akijifunza. Kwa muda mfupi Migueli aliweza kuimba wimbo ule pamoja na Maria.

Shughuli ya 1: Kuchunguza ujifunzaji wa asili

Kabla ya kuanza shughuli hii, soma Nyenzo Rejea 2: Utafiti juu michezo ya jadi katika mtalaa . Nyenzo rejea hii inaeleza kazi moja ya utafiti na micezo miwili ambayo walimu waliibuni kama matokeo ya utafiti huo. Kusoma pia Nyenzo Rejea Muhimu: Kufanya utafiti darasani kutasaidia sana. Zungumza na wanafunzi wako kuhusu ujifunzaji. Je, wanajua kwamba daima hujifunzia: nyumbani, shuleni, wakati wanapocheza?
Liambie darasa lifanye uchunguzi katika ujifunzaji wa ‘asili’. Swali lao ni: Ujifunzaji gani unaotokea wakati watoto wanapocheza? Wanafunzi lazima waandike na kuchora kuhusu ujifunzaji wanaouona kwenye uwanja wa michezo na baada ya kutoka shule, wakati wanafunzi wengine wanapocheza, na wanapocheza wao wenyewe.
Wwaambie wanafunzi darasani washirikishane matokeo yao, kwenye vikundi. Kiambie kila kikundi kioneshe jinsi ya kucheza mchezo mmoja. Rekodi nyimbo au mikarara/viitikio wanavyoimba wakati wa mchezo, kwenye tepu, au kwa kuandika.
Waambie wanafunzi kwenye kila kikundi wajadili kile ambacho wanaweza kujifunza kutokana na michezo hii. Andika mawazo yao.
Umejifunza nini kutokana na shughuli hii inayohusu namna michezo inavyoweza kusaidia katika ujifunzaji?

Somo la 2

Aina zote za michezo zinaweza kutumika kwa kujifunzia na unahitaji kufikiri kiubunifu jinsi ya kuitumia michezo darasani (angalia Shughuli 2). Inasaidia kama unaweza kushirikiana na wenzako pamoja na rafiki zako, na pia kushirikiana na wanafunzi wako, katika kubuni mawazo mapya ambayo yanaweza kufanya ujifunzaji darasani kwako uwe wa kufurahisha na wenye mafanikio.
Katika sehemu hii, wewe na darasa lako panueni utafiti wenu kwa kuwauliza wanajumuiya kuhusu michezo waliyokuwa wanaicheza walipokuwa wadogo.

Uchunguzi kifani ya 2: Michezo na mikarara/viitikio katika kadi za kusoma

Kuna ongezeko la kupenda lugha nyingi za nyongeza katika mitalaa kote Afrika. Hii ina maana kuna ujifunzaji wa awali unaotumia lugha mama, na lugha nyingine za nyongeza (bila kuchukua nafasi ya ile lugha mama). Mtalaa unalenga kuingiza lugha zote ambazo watoto wanazijua wakati wa masomo yao.
Bwana Maleke mkoani Lindi hutumia shughuli ifuatayo, ambayo hujumuisha lugha nyingi za nyongeza, pamoja na wanafunzi wake wa darasa la 5. Humpatia kila mwanafunzi kipande cha kadi. Wanafunzi huchora picha katika upande mmoja wa kadi. Kwa upande mwingine, huandika nyimbo, michezo, mikarara/viitikio au mashairi, ambayo wanayapata nyumbani.
Kila siku, wana kipindi cha kusoma ambapo wanafunzi wanasoma (au wanaimba!) kile kilichoandikwa kwenye zile kadi. Wakati mwingine, msomaji bora husoma kadi na msomaji anayesoma polepole zaidi. Wakati mwingine, mzungumzaji wa lugha moja, humsaidia mwanafunzi mwingine kusoma lugha yake na kuingiza sauti. Wakati mwingine, wanaigiza hayo mashairi au wanacheza michezo hiyo. Bwana Maleke amegundua jinsi darasa lake linavyokuwa na furaha na jinsi wanafunzi wanavyoshirikiana vizuri katika mazungumzo na wanavyochanganyika vizuri zaidi tangu waanze kufanya hivi.

Shughuli ya 2: Michezo na nyimbo kutoka kwa wanajumuiya ambao ni watu wazima

Waambie wanafunzi wako wamwombe mtu mzima (mzazi, babu/bibi, jirani n.k.) awafundishe mchezo, wimbo au mkarara ambao walikuwa wakiufurahia wakati wa utotoni. Wanatakiwa wajue kanuni za maneno na nyenzo zozote ambazo zinahitajika.
Siku inayofuata, orodhesha michezo na nyimbo ambazo wanafunzi wamezileta toka nyumbani.
Waweke pamoja wanafunzi wanaojifunza mchezo au wimbo wa aina moja. Waambie wajiandae kufundisha darasa mchezo au wimbo huo.
Waambie waandike huo wimbo au huo mkarara au wacheze mchezo wa kwenye kadi.
Darasa litakapomaliza kujifunza mchezo au wimbo huo, jadilianeni kitu ambacho wanaweza kujifunza kutokana na mchezo au wimbo huo. Andika tini kama ulivyofanya hapo awali.
Kwa masomo yatakayofuata, wahamasishe wanafunzi wasome magazeti ili kutafuta nyimbo, michezo, vitendawili na mizaha kama msingi wa kuandika vitu vyo wenyewe.

Somo la 3

‘Kuakisi’ ni kutafakari juu ya kile kilichotokea na kuona jinsi ya kufanya vizuri zaidi wakati mwingine. Baada ya kuwa umejaribu shughuli mpya, inasaidia sana kuakisi/kutafakari juu ya mafanikio na kitu gani kinahitaji maboresho. Fanya mchakato wa ‘Panga-Tenda-Rekodi-Tafakari’ kuwa sehemu ya mazoea yako ya kila siku (angalia Nyenzo Rejea 1 ).
Sasa una mkusanyiko mzuri wa michezo, unaweza kuitumia michezo hii kama msingi wa shughuli za ujifunzaji, na kama msingi wa kuakisi/kutafakari na uboreshaji. (kazi hii pia inaweza kufanywa kwa kutumia hadithi.)
Nyenzo Rejea 3: Michezo ya maneno ina michezo kadhaa ambayo unaweza kuijaribu pamoja na wanafunzi wako.

Uchunguzi kifani ya 3: Vitenzi vya Kiswahili katika wimbo wa kurukaruka maneno

Bi Alison aliimba wimbo wa kurukaruka maneno wakati alipokuwa mtoto pale Mazimbu, Morogoro. Aliamua kuutumia wimbo huo kufundishia wanafunzi wake wa darasa la 2 maneno kadhaa na virai vya wakati uliopo vya Kiswahili.
Kwanza wanafunzi waliuimba kwa Kiswahili na kisha aliwasaidia kuuimba kwa Kiingereza.
Alimpatia kila mwanafunzi kipande cha karatasi chenye kitenzi (m.f. la, nywa, cheka, kohoa, ruka, kimbia, rukaruka) kilichoandikwa kwenye karatasi hiyo. Alihakikisha kuwa kila mtoto anafahamu maana ya neno hilo na jinsi ya kufanya vitendo vinavohusiana na neno hilo.
Alimwambia kila mwanafunzi mmoja mmoja afanye vitendo bila maneno, na darasa liliimba ubeti mpya: ‘Antoni, msichana huyu anafanya nini? Antoni, msichana anacheka,’ n.k.
Baada ya somo, alitafakari kuhusu:
Kile kilichokwenda vema;
Kile ambacho hakikwenda vema sana;
Kile kilichomshangaza;
Kile ambacho angekibadili kama angerudia lile somo.
Bi Alison alishangazwa na jinsi wanafunzi walivyoutumia muda katika kujifunza toleo la Kiswahili lakini pia jinsi wanafunzi waliufurahia muda. Aliona kuwa alihitaji kutumia muda zaidi katika shughuli hii, na pia kufundisha maneno machache zaidi.
Wiki iliyofuata, alitumia toleo la aina nyingine la Kiswahili lililokuwa na wimbo wa kurukaruka maneno kwa jinsi ile ile, ya kutunga beti zenye aina mbalimbali za vyakula.
(Angalia Nyenzo Rejea 4: Wimbo wa kurukaruka maneno kutoka katika wimbo wa kurukaruka maneno wa Igbo.)

Shughuli muhimu: Kujifunza kutokana na mkarara, wimbo au mchezo

Je, kuna mkarara kwenye makusanyo ya darasa lako ambao lugha yake inaweza kubadilishwa na kuwa kama lugha ya nyongeza na kuweza kutumiwa katika kuhamasisha ujifunzaji wa lugha?
Bainisha sentensi katika mkarara ambayo neno (au maneno) yangeweza kubadilishana nafasi kwa zamu. Kwa mfano, ‘Anacheka’ lingeweza kubadilishana nafasi na (Anaruka, anarukaruka, anakimbia’ n.k.). Kila mwanafunzi, au kikundi, kinaweza baadaye kuimba ubeti mpya, wenye neno jipya katika sentensi ya mwanzo.
Ingeweza hata kufurahisha zaidi kama maneno au sentensi yataweza kuambatana na vitendo.
Panga jinsi utakavyopanga darasa lako kwa ajili ya kuimba/ kukariri na kuigiza (zoezi hili ni mbadala’. (Huu ni mfululizo wa sentensi, ambazo zinafanana isipokuwa kwa neno au kishazi kimoja. Sentensi hizi zinatumika kufanya mazoezi ya mitindo ya lugha.)
Kama hutafanikiwa, utatakiwa kujaribu wimbo mwingine, au njia nyingine ya kuendesha shughuli hii.

Nyenzo-rejea ya 1: Duara la tenda – tafakari

 Nyenzo-rejea ya mwalimu kwa ajili ya kupanga au kutohoa na kutumia na wanafunzi.
Mpendwa …………………
Darasa letu la …… linajifunza kuhusu hadithi za asili na stadi za kusimulia hadithi. Tumesikia kuhusu ubingwa wako na tunapenda kukukaribisha kuja na kutusaidia kujifunza ni namna gani tunaweza kukuza stadi zetu za kusimulia na kujifunza hadithi pia.
Tungependa uje …………………………………. Tafadhali tujulishe kama muda huu ni mwafaka kwako. ………………………………… kutoka katika darasa letu atakusubiri geti la shule saa 4.00 asubuhi.
Tunashukuru sana

Darasa la 5
Shule ya Msingi ya Mtakatifu Maria

Nyenzo-rejea ya 2: Tathmini uigizaji wa hadithi za vikundi

Usuli/welewa wa somo wa mwalimu


Kielelezo kinaonesha hatua zifuatazo katika mduara wa tenda- Akisi/Tafakari:
Panga shughuli.
Tenda kwa kuweka mpango katika vitendo, na chunguza unavyoendelea.
Rekodi kile unachokiona.
Akisi/Tafakari juu ya kilichotokea.
Pitia tena mpango wako, au andaa mpango mpya.
Weka mpango uliopitiwa tena au mpango mpya katika vitendo, na angalia tena.
Rekodi na tafakari tena.
Na kadhalika, na kadhalika …
Kila kitu unachokifanya kama mwalimu kinaweza kuwa sehemu ya mduara wa
Tenda -Tafakari.
(Angalia pia Nyenzo Rejea Muhimu: Kufanya utafiti darasani)

Nyenzo rejea 3: Utafiti juu ya michezo ya jadi katika mtalaa

Usuli/welewa wa somo wa mwalimu
Nonhlanhla Shange alifanya utafiti katika Shahada yake ya Uzamili katika Kitengo cha Usomeshaji wa Vijijini cha Nelson Mandela katika Chuo Kikuu cha Fort Hare nchini Afrika Kusini. Alitafiti kuhusu utumizi wa michezo ya jadi darasani, utafiti ambao aliufanya katika shule nne za vijijini.
Wanafunzi na walimu wao walifanya utafiti wa vitendo katika michezo ya jadi.
Walimu walisikiliza kwa makini na waliandika tini za michezo ambayo wanafunzi waliileta darasani. Walijaribu kutayarisha masomo yanayohusu michezo hii. Wanatunza juzuu, ambamo huwekwa kumbukumbu za masomo haya, na kujaribu kufanya maboresho kwa ajili ya matumizi ya baadaye.
Maelezo ya michezo miwili ambayo ilichezwa kama sehemu ya utafiti huu ni haya yafuatayo hapa chini.
1. Mchezo wa duara
Matayarisho ya mchezo huu yanajumuisha uchoraji wa kielelezo kama hiki hapa chini ambacho huchorwa ardhini.


Mchezo unachezwaje?
Mchezo huu unachezwa kwa vikundi vidogo vya wanafunzi watano watano au sita sita. Mwanafunzi mmoja anarukia ndani ya nafasi za duara, akigeuka upande hadi upande, wakati wanafunzi wengine wakiimba wimbo mfupi au shairi fupi, kwanza kwa lugha ya asili, na kisha kwa Kiswahili.
Shughuli gani za ujifunzaji zilizohusiana na mchezo huu?
Mchezo ulibuniwa ili kuonesha ni jinsi gani kurudia rudia kwa kutumia lugha ya wanafunzi wenyewe na lugha ya Kiswahili kunavyoweza kusaidia katika kujifunza. Kwa kutumia wimbo mfupi au shairi, mchezo huu pia uliweza kutumika katika kuwafundisha wanafunzi kuhesabu.
2. Mcezo wa mawe
Matayarisho kwa ajili ya mchezo hujumuisha uchoraji wa duara chini ardhini na kuweka idadi fulanii ya mawe kwenye duara hilo. (duara lisizidi kipenyo cha mita moja.)


Mchezo unachezwaje?
Wanafunzi wanagawanywa katika vikundi vya watano watano au sita sita. Kila kikundi kinakuwa na duara lake lililochorwa ardhini na kuwekwa mawe ndani yake.
Mchezaji anarusha jiwe moja juu; kabla halijatua ardhini, lazima wajaribu kuokota mawe mengine ndani ya duara.
Kila mwanafunzi katika kikundi lazima ajipe namba mwenyewe (chini ya 10). Namba hii ni idadi ya mawe ambayo mchezaji atajaribu kucheza na kuokota.
Mchezaji mmoja anaingia kwanza. Kama mchezaji huyu ataokota idadi ya mawe inayotakiwa kutoka kwenye duara, wanasema orodha ya kuzidisha ya namba hii (kwa mfano, orodha ya 3 ya kuzidisha, wanakomea kwenye 30 – hii inaweza kuwa ni ya chini kwa wanafunzi wadogo zaidi).
Kama mchezaji atashindwa kuokota idadi inayotakiwa ya mawe kutoka kwenye duara, watapaswa kuzidisha idadi ya mawe waliyookota kwa idadi ya mawe ambayo walipaswa kuokota, na kupata jibu sahihi. Kwa mfano, kama walitakiwa kuokota mawe hadi 5, lakini wakaokota mawe 3 tu, watatoa jibu sahihi la 5 x 3.
Wachezaji wengine watapima/watajaji endapo wametoa jibu sahihi au jibu ambalo si sahihi.
Shughuli gani za ujifunzaji ambazo zinahusishwa na mchezo huu?
Mchezo huu ulitumiwa ili kuwafanyia wanafunzi mazoezi ya ’ stadi’ za kuzidisha.
Chanzo cha Asilia: Shange, N., Kitengo cha Mfuko wa Nelson Mandela wa Usomeshaji na Maendeleo ya Vijijini [ utafiti haujachapishwa ] Nelson Mandela Foundation’s Unit for Rural Schooling and Development [unpublished research]

Nyenzo rejea 4: Michezo ya maneno

Nyenzo rejea ya mwalimu kwa ajili ya kupanga au kurekebisha ili kutumia na wanafunzi
Michezo hii inaweza kuchezwa kwa kutumia lugha yoyote na kwa umri wowote, ilimradi tu wanafunzi wanajua vizuri stadi za kusoma na kuandika.
Mchezo 1: Bingo
Wasomee wanafunzi hadithi wanayoipenda na waambie wachague maneno mawili wanayoyataka.
Mwulize kila mwanafunzi maneno yao na andika maneno muhimu ubaoni ambapo kila mmoja ataweza kuona.
Ligawe darasa katika vikundi vya wanafunzi sita sita na kiambie kila kikundi kichague maneno 12 kwa ajili ya kikundi chao. Haya yanaweza kutofautiana kwa kila kikundi.
Kila mwanafunzi atengeneze karatasi ya bingo kwa kuchora mraba mkubwa uliogawanyika katika miraba midogo tisa (angalia mfano hapa chini).
Mwambie kila mwanafunzi achague maneno yoyote tisa kutoka kwenye orodha yao ya maneno 12 na kuyanakili katika karatasi yao ya bingo, neno moja kwa kila mraba. Makaratasi ya wanafunzi yatakuwa tofauti, kwa sababu wataweza tu kuchagua maneno tisa kati ya maneno 12.
Mwanafunzi mmoja atakuwa na karatasi kuu yenye maneno 12. Watatoa maneno bila mpangilio maalum. Neno linavyotajwa kila mwanafunzi ambaye atakuwa na neno hilo katika karatasi ya bingo atatakiwa kulikata. Wa kwanza kukata maneno yake yote atapiga kelele ‘Bingo’ na atakuwa ameshinda.
Kiache kila kikundi kicheze tena na kila mwanafunzi apate zamu ya kutaja maneno.
Kama unataka kutumia karatasi ya bingo zaidi ya mara moja, waambie wanafunzi wazibe maneno hayo kwa mawe au vihesabio wakati wa kutaja maneno.
Je, wanafunzi walijifunza maneno mapya? Unajuaje?
Orodha ya Sampuli ya maneno kwa ajili ya Bingo:
Ndizi
Maharage
Kabeji
Mihogo
Nazi
Punje za mahindi
Maembe
Mahindi
Machungwa
Mapapai
Mapeasi
Spinachi
Viazi vitamu
Mifano miwili ya kadi za bingo:
Mchezo 2: Maneno yanayohusu supu
Tengeneza orodha ya maneno tisa, mf. sehemu za mwili, vyumba vya nyumba, au mboga za majani. Weka orodha hii ubaoni (pembeni mwa picha toa maelekezo ya maneno kama unaweza).
Mpatie kila mwanafunzi kipande cha karatasi cha mraba, herufi moja kwa kila mraba. Waambie waingize maneno muhimu katika karatasi hiyo kwenye miraba hiyo, herufi moja kila mraba mmoja. Waambie kuwa maneno yanaweza kutoka kushoto kwenda kulia, au juu mpaka chini. Waambie wanafunzi wajaze miraba ya ziada kwa herufi zozote zile za alfabeti. (Angalia mfano hapa chini).
Kila mwanafunzi akishafanya hivi, kusanya makaratasi yote na yachanganye. Sasa wagawie wanafunzi makaratasi hayo bila mpangilio maalum, na waambie wanafunzi wazungushie maneno yote wanayoweza kuyapata. Kila mwanafunzi anajua lazima maneno yawe tisa. Wa kwanza kumaliza ndiye mshindi.
Wanafunzi wanaweza baadaye kuchagua somo lao wenyewe au eneo lao wenyewe na maneno yanayohusu supu kutoka kwenye orodha hii na kumpatia rafiki acheze.
Mfano wa maneno yanayohusu supu
Maneno ya kutafuta kwenye maneno ya supu
Mbuzi  Ngamia
Simba Twiga
Nyoka Nyani
Chui  Farasi
Unaweza kufanya shughuli hii iwe ya kusisimua zaidi kwa kuwauliza ‘Neno gani ambalo LINALOHUSIKA katika supu?’ Unaweza kutumia mchezo huu kwa maneno mengi mbalimbali na kwa masomo mbalimbali.
Kiolezo wazi kwa ajili ya maneno ya supu ni hiki hapa chini. Unaweza kuongeza miraba zaidi au kuifanya iwe midogo zaidi ili kufanya mchezo uwe mgumu zaidi au mrahisi zaidi kutegemeana na umri na uwezo wa wanafunzi wako.

Nyenzo Rejea 5: Wimbo wa kurukaruka maneno

Nyenzo rejea ya mwalimu kwa ajili ya kupanga au kurekebisha ili kutumia na wanafunzi
Wimbo wa Kiigbo wa kurukaruka maneno Ikuku buru gi
Zamiriza
Buru gi buru nwa nnegi
Zamiriza
Nwa nnegi idobere na ukwu osisi kporonku
Chọ ya ịhuyi ya (2x)
Tafsiri ya Kiswahili
Acha upepo ukupeperushe
Zamiriza
Ukupeperushe wewe na mdogo wako wa kike
Zamiriza
Yule mdogo wako wa kike yupo chini ya mti wenye matawi yote yenye kivuli
Unamtafuta mdogo wako huyo, huwezi kumpata (x2)

FASIHI YA DAYALOJIA KATIKA KAZI ZA FASIHI

Eleza dhima ya dayalojia katika kazi za fasihi ukitoa hoja madhubuti.

Katika kazi za Fasihi dayalojia hutumiwa zaidi katika tamthiliya ingawa hujitokeza pia katika kazi za Fasihi kama riwaya. Utokeaji wa dayalojia hufanya kipengele hiki kionekane kuwa na umuhimu wa pekee na kuleta ulazima wa kuchambua umuhimu wake. Umuhimu wa dayalojia ni kama ufuatao:
  1. Husaidia kuitambulisha kazi ya Fasihi kuwa ni tamthiliya kwa msingi wa ki-Aristotle tamthiliya ni lazima itawaliwe na majibizano (dayalojia).
  1. Kuiwezesha kazi ya tamthiliya kuigizika jukwaani kwa sababu tamthiliya zote ni sanaa za maonesho hivyo ni lazima ziwe katika majibizano ili kuweza kuwapata waigizaji.
  1. Kuipa kazi ya Fasihi muundo wa kimgogoro ambao utaonesha msuko wa visa kimgogoro na kubainisha kwa urahisi chanzo cha mgogoro, kukua kwa mgogoro, kilele cha mgogoro, kushuka kwa mgogoro na suluhisho la mgogoro.
  1. Dayalojia husaidia kuleta uhalisia wa matukio yanayofikishwa na mtunzi, kwa mfano kupitia majibizano ya wahusika tunaweza kubaini hali halisi iliyopo ndani ya jamii kwa urahisi kama inavyojitokeza kupitia “Mama Suzi” na “Baba Joti” wanaoamini kuwa dini na mila haziruhusu kuzungumzia masuala ya mahusiano ya kimapenzi kwa watoto huku “Baba Anna” na “Mjomba” wakiamini juu ya utoaji wa elimu. Lakini pia dayalojia kati ya “Jirani” na “Baba Joti” inasaidia kugundua jinsi wanajamii wasivyoamini juu ya kuwepo kwa janga la UKIMWI na badala yake wanaamini kwenye nguvu za kishirikina.
  1. Dayalojia pia hutumika kuishirikisha hadhira na kuifikirisha kwa kuvaa uhusika kupitia majibizano ya wahusika anaowasoma katika kitabu.
  1. Dayalojia husaidia kupambanisha fikra na mitazamo tofauti ndani ya jamii ambayo kimsingi huathiri mwelekeo mzima wa jamii kujiletea maendeleo kwa ufano imani potofu juu ya malezi ya vijana waliozama katika kizazi cha utandawazi dhidi ya malezi ya vijana wa zama za kale ambao walitishwa kwa miiko ya kijamii tu na wakatii. Hapa unaona wanachoamini “Baba Joti” na “Mama Suzi” dhidi ya wanachokiamini “Mjomba”na “Baba Anna” kuhusu malezi na haja ya jamii kubadili mbinu za malezi ili kuendana na jamii ya sasa.
Kwa ujumla dayalojia ni kipengele muhimu sana katika kazi ya Fasihi hasa tamthiliya kwani pamoja na mambo mengine lakini hipa uhalisia zaidi kazi ya Fasihi na kuchochea tafakari ya mambo yalivyo katika jamii.

Monday 9 September 2019

UHAKIKI WA RIWAYA YA WASIFU WA SITI BINTI SAAD-----Na Shaaban Robert

UHAKIKI WA DIWANI YA FUNGATE YA UHURU------Na Mohamed S. Khatibu --------1988-------- ( DUP )

WASIFU WA SITI BINTI SAAD-----RIWAYA / HADITHI--------BY SHAABAN ROBERT

Siti binti Saad alikuwa mwanamke wa kwanza Zanzibar kusimama jukwaani na kuimba nyimbo za taarab. Katika kitabu hiki, Shaaban Robert anaelezea juu ya maisha ya umaskini na hali ya chini aliyoishi msanii huyu, katika jamii ya Zanzibar iliyokitwa na tabaka za kijamii miaka ya kwanza ya karne ya ishirini. Licha ya kuwa sura yake ati haikuwa nzuri, alifikia hali ya juu ya nyota wa uimbaji wa taarabu akapendwa na wapenda taarabu si Zanzibar tu na Afrika ya Mashariki, lakini pia alipendwa hadi Misri na India. Kwa wapenzi wa taarab bado ni malkia, sawa na alivyokuwa Om Kulthum wa Misri. 
 
 Siti binti Saad was the first woman Taarab singer in Zanzibar. In this book Shaaban Robert looks at the background of the singer: poverty and low birth, in a society riven by class and race in early 20th century Zanzibar. Despite her so-called bad looks, she became a star whose voice was recognised and loved by many, not only in Zanzibar and East Africa, but as far as Egypt and India. She was and remains to taarab lovers, the equivalent of Egypt’s Om Kulthoum.

Saturday 7 September 2019

SHAIRI : LOLIONDO KWA BABU


Habari natangazia, Kuwapatia uhondo Nchini Tanzania,   Kijiji cha  Loliondo
Watu viguu na njia, Wanoenda kwa vishindo
Kiongozi wa kanisa, Siku hizi anaganga
Siku imepambazuka, Naamshwa kwa kelele
Najifunga yangu shuka, Kutazama walo mbele
Tayari washazunguka, Kwa Kasisi Ambakile
Kiongozi wa kanisa, Siku hizi anaganga
Miujiza imefika,  Babu yeye keshaota
Wote mloathirika, Anzeni kujikokota
Loliondo mkifika,  Mizizi inatokota
Kiongozi wa kanisa, Siku hizi anaganga
Iwapo una nafasi,  Usiende mhimbili
Ondoa na wasiwasi, Loliondo kuna dili
Dawa bei ni rahisi, Kikombe ni buku mbili
Kiongozi wa kanisa, Siku hizi anaganga
Kashinda madakitari, Walosoma hadi ng’ambo
Magonjwa yote hatari, Yalokuwepo kitambo
Eti mpaka kisukari,  kweli babu ana mambo
Kiongozi wa kanisa, Siku hizi anaganga
Ukimwi unatutisha, Ugonjwa kama adhabu
Waganga wamechemsha, Kutafuta matibabu
Kama mbinu zimekwisha, Kajaribuni kwa babu
Kiongozi wa kanisa, Siku hizi anaganga
Kwa babu kuna vioja, Kabla kutoa tiba
Hutangaza yake hoja, Dawa msije kuiba
Mnapata mara moja, Sio kunywa mkashiba
Kiongozi wa kanisa, Siku hizi anaganga
Wala msifanye pupa,  Walokwenda ni umati
Babu dawa akikupa,  Kunywa  kwa kombe la bati
Usipeleke na chupa, Ukayavunja  masharti
Kiongozi wa kanisa, Siku hizi anaganga
Aponya kila madhara, Hili wengi wanakiri
Pengine ni  biashara, Katumia muhubiri
Kujitoa  ufukara,  Ajipe na utajiri
Kiongozi wa kanisa, Siku hizi anaganga
Mara bibi wa tabora, keshaibuka na yake
Kujiona ndio bora, Na yeye afaidike
Watu kweli ni wakora, Jamani tuwajibike
Kiongozi wa kanisa, Siku hizi anaganga
Sijui kama ya kweli, Msije mkasusia
Mi nahisi utapeli,  Mbuzi ndani ya gunia
Dawa sijaikubali,   Maajabu ya dunia?
Kiongozi wa kanisa, Siku hizi anaganga
Namefika kaditama,  Dawa zinanitatiza
Babu ataniandama,  Malenga kuniapiza
Ninaogopa lawama,  Shairi nimemaliza
Kiongozi wa kanisa, Siku hizi anaganga
HAMZA A. MOHAMMED